Tuesday 3 February 2009

Wizi Mtupu

Matukio nchini Tanzania ya miaka ya hivi karibuni ni matunda ya jitihada kubwa ambazo zimefanywa na kundi dogo la Watanzania miaka iliyopita kuhujumu rasilimali za Taifa kwa kiwango cha hali ya juu kabisa. Kwa msemo mwingine, kwa kiwancgo cha lami.

Leo kila kukicha, tunasoma habari kuhusu namna ambavyo Watanzania hawa, wengi wao ambao ama walikuwa viongozi wenye nyadhifa mbalimbali Serikalini, au ni watu waliyokuwa na uhusiano na voingozi Serikalini, walivyopanga mipango mbalimbali kuchota pesa za umma kwa manufaa yao binafsi.

Baba lao kati ya hizi njama inajulikana kama kashfa ya EPA ambayo inahusisha kundi la walaji kuchota pesa zilizokuwa kwenye akaunti maalum ya kulipa madeni nje ya nchi, pesa ambazo zilikuwa zikisubiri upatikanaji wa fedha za kigeni ili zitumwe kwa makampuni ya nje ambayo yalikuwa yameuzia kampuni au mashirika ya Tanzania bidhaa mbalimbali.

Wajanja wakaamua kukwapua hizo pesa na leo hii, polepole, zinaendelea kufichuka habari kuhusu wizi huo wa mabilioni ya pesa.

Jambo la kustaajabisha ni kuona jinsi gani hawa Watanzania walipata ujasiri wa kuendesha vitendo hivi kinyume na sheria bila woga kuwa siku za mwizi siyo bilioni moja, ni arobaini tu.

Chama tawala, Chama cha Mapinduzi (CCM) hakina budi kuchukuwa hatua zaidi dhidi ya watuhumiwa siyo wa wa EPA tu lakini wa kashfa nyingine zote ambazo siyo tu zinatishia kuendelea kwa CCM kuongoza Serikali, hasa tukizingatia kuwa uchaguzi mkuu wa 2010 unakaribia, lakini kutochukuwa hatua madhubuti kunaweza kuhatarisha uhai wa nchi na hata usalama wake. Wananchi wanapokosa imani juu ya uwezo wa Serikali wa kutetea maslahi yao na ya nchi huwa wako tayari kuchukuwa hatua ambazo zinapingana na sheria.

Hivi karibuni shekhe mmoja wa Mwanza ametamka kuwa haina haja kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wa mauaji ya albino. Alisema wakamatwe, wafikishwe hadharani, na wapigwe risasi. Serikali ya CCM isipochukuwa hatua madhubuti kupunguza tsunami hii ya rushwa, mamneno ya huyo shekhe yataanza kuonekana halali kutumika dhidi ya watuhumiwa wa kashfa lukuki za rushwa ambazo zinaindama Tanzania.

Rais Kikwete alitamka mjini Tanga miaka michache iliyopita kwa utaratibu unaoruhusu viongozi kuwa na maslahi ya kibiashara umepunguza imani ya wananchi kwa viongozi na Serikali yao. Tatizo limeonekana, na dawa inajulikana. Labda mdunga sindano na mambomba ya sindano ndiyo vinakosekana.

Saturday 3 January 2009

Angekuwepo Juliasi…

Ni dhahiri kuwa Mwalimu Nyerere angekuwa yuko Tanzania leo hii, kiwango cha tuhuma za ufisadi tunachokiona Tanzania hivi leo kisingeonekana. Kwa sababu hakuwa kiongozi wa kunyamazia viongozi wanaovunja maadili na dhamana wanayopewa na wananchi.

Kwamba kiongozi haoni aibu kukiri kuwa ana 'vijisenti' vipatavyo dola milioni moja kwenye akaunti yake binafsi ni kielelezo cha nyakati zetu za sasa. Haya yasingeweza kutokea kwenye serikali ya awamu ya kwanza, na yasingeweza kutokea kwenye Serikali hii kama Nyerere angekuwepo.

Pamoja na porojo tunazoambiwa na viongozi wetu kuhusu nia yao kubwa ya kumuenzi Nyerere, ukweli ni kuwa hawafanyi hivyo. Na pengine ni kweli kuwa wanajuta kuzaliwa kwenye nchi moja na Nyerere. Kwa sababu ndiye tunayemtumia kuwapima viongozi waliyomfuata. Na ndiyo hayo yanayowafanya Watanzania wengi kuona kuwa tuhuma za sasa dhidi ya viongozi wetu zinavunja imani ya wananchi juu ya viongozi wao, na zinahatarisha amani ambayo tunaambiana bado iko Tanzania.

Na siyo yeye tu, tunawapima pia kwa kuwalinganisha na viongozi wengine kama Mwinyi, Sokoine, Kawawa, Msuya, Warioba, na wengine. Sina maana kuwa hawa wote wana sifa zinazofanana. Hoja ni kuwa kitu au mtu hawezi kuwa mbaya au mzuri bila kulinganishwa na mtu mwingine.

Miaka 100 kutoka leo Watanzania watashindwa kutofautisha kati ya aina ya viongozi wenye vijisenti kwenye visiwa vya ughaibuni, na wananchi ambao hawakuchukuwa hatua yoyote ile kurudisha uadilifu kwenye uongozi wa nchi yao ili kuondokana kabisa na viongozi wa aina hiyo.

Au labda hili nalo linahitaji wafadhili?

Sunday 9 November 2008

Serikali inatuangusha

Kuna habari zilitangazwa Mei 2008 kuwa Serikali ya Tanzania itachukuwa hatua za kisheria dhidi ya kampuni ya Norconsult kwa tuhuma kadhaa, ikiwa ni pamoja na kuendesha biashara bila kuandikishwa, na kukwepa kulipa kodi.
 
            Habari kamili :
            http://allafrica.com/stories/200805090429.html
 
Kuna msemo wa Waingereza: Closing the stable door after the horse has bolted. Una maana kitendo cha kuchukuwa hatua baada ya athari kutokea.
 
Norconsult imefanya kazi Tanzania bila kuandikishwa kwa miaka kumi bila bugudha. Inakisiwa kukwepa kodi zipatazo Sh.2.4 bilioni. Imeshinda kandarasi kusimamia miradi mikubwa ya ujenzi ikiwa ni pamoja na barabara ya Sengerema - Busagara (Sh.35.7 bilioni), na barabara ya Marangu - Rombo Mkuu (Sh.23.3 bilioni).
 
Haiingii kichwani kuwa kampuni imepata kazi kubwa kama hizo Serikalini na hamna mamlaka yoyote iligunduwa kuwa kuna walakini. Kwa miaka kumi!
 
Hapa kinachoonekana kutokea ni makundi yenye maslahi ya kisiasa na uchumi yameanza kupambana kwa kutoleana siri zao. Na hii inatokea sana kwenye mifumo ya siasa ambapo kundi moja likishinda uchaguzi hutokea kujaribu kuhodhi madaraka yote ya kisiasa, kiuchumi, na kijamii na kusababisha kundi lililonyimwa fursa linapoingia madarakani kulipiza kisasi.
 
Kuna msemo wa Kiswahili: Vita vya panzi ni furaha ya kunguru. Msemo unaofaa katika mazingira haya ni: Kunguru (wakubwa) wakigombana, panzi (raia) wanapata ahueni.

Friday 31 October 2008

Nchi Inakwenda Kombo

Pamoja na kwamba Serikali inasema mambo yanakwenda vizuri, ukweli ni kuwa Serikali inaelemewa na matatizo ya kila aina.

Migomo ya walimu, ya wanafunzi, ya wafanyakazi. Kushindwa kwenye uchaguzi mdogo wa jimbo la Tarime, na hivi karibuni wastaafu wa Shrika la Bandari kuvua nguo barabarani wakishinikiza Serikali kulipwa mafao yao.

Serikali ikiendelea kujidanganya kuwa hakuna tatizo, itaendelea kupoteza majimbo ya uchaguzi kwenye Uchaguzi Mkuu 2010.

Wednesday 29 October 2008

Kimya Kikubwa Kina Mshindo

Nimekuwa kimya kwa muda, lakini nitaanza tena kuandika kwenye blog hii baada ya muda si mrefu.

Yako mengi ya kusema, lakini nitachagua yale muhimu katika kuchangia mawazo mbalimbali.

Saturday 10 May 2008

Robert Gabriel Mugabe

Hawapo wengine watakofuata nyayo za kina Mugabe.

Ni kweli, Mugabe amechelewa kuchukuwa hatua zilizoifikisha Zimbabwe hapo ilipo lakini ukweli ni kuwa kosa lake kubwa ni kupingana na Wamarekani na Waingereza, na suala zima la vikwazo vya uchumi dhidi ya Zimbabwe kwa sababu ku kutokubali kwake kuimba ngonjera zinazotungwa Washington na London.

Viongozi wa kizazi kipya, wakina Tsvangirai, haiwasumbuwi kuweka maslahi ya nchi pembeni kwa kisingizio cha

Saturday 26 April 2008

Wanaanza kuanguka, mmoja baada ya mwingine.

Alianza Edward Lowassa, akafuata Ibrahim Msabaha, na muda haukupita, Nazir Karamagi akaaachia ngazi.

Kwa kasi hii, tunaweza kufika mwaka 2010 ikawa hatuna kiongozi hata mmoja ambaye hajaguswa na Kiwanda cha Kashfa cha Tanzania (KKT).

Niliwahi kutabiri, bila kuwa na ushahidi madhubuti, kuwa itakapofika 2015 Tanzania itakuwa na nafasi ya kupata Rais safi, ambaye hana kashfa wala marafiki wenye kashfa, na ambaye hataogopa kuchukuwa hatua dhidi ya wale wenye tuhuma za kashfa.